Kuna watu ambao kila siku wanainua mataifa bila kupanda jukwaani. Watu wanaojitoa, lakini hawatajwi. Watu waliojaa majeraha ya ukimya, lakini bado wanatabasamu. Leo, Palubongo tunakuletea hadithi ya shujaa tuliyemzoea sana kiasi cha kumsahau Mwalimu wa Shule ya Msingi. Asubuhi ya Maisha Yake Ni saa 11 alfajiri, kijiji cha Ng’ongo bado kimejaa giza. Ukisikiliza kwa makini, utasikia sauti ya sufuria ikigongana na jiko la mkaa. Mwalimu Rehema, mama wa watoto watatu, anapika uji wa mahindi kwa haraka kabla hajavaa kitenge chake cha bluu na kusafiri kwa miguu kilomita nne kwenda kufundisha darasa la pili. Barabarani, atakutana na maji ya mvua yaliyotuama, na wakati mwingine mbwa wa mtaani watamtisha. Lakini kila hatua anayoipiga, anaiona kama sala ya kimya kwa ndoto za watoto wake wa darasani. Anapoingia shule saa 1:30 asubuhi, hakuna chai, hakuna ofisi yenye kiyoyozi, hakuna kompyuta. Lakini kuna ubao, chaki, na watoto 72 waliokaa kwenye madawati yaliyopasuka, wakimsubiria s...