Ruka hadi kwenye maudhui makuu

Urafiki: “Msaada Bandia Umefichuliwa”

 

 “Kuna marafiki wa kula, marafiki wa kucheka, na wachache sana wa kulia nao usiku wa manane. Wengi huvaa ngozi ya urafiki, lakini ndani wana ajenda zao. Ukweli huu unauma, lakini ni lazima usemwe.”

Ndoto ya Urafiki wa Kweli:

Tunaota kuhusu urafiki tangu utotoni, wakati tulikuwa tunagawana pipi za kijiti shuleni au kukimbizana uwanjani bila sababu ya maana. Tuliamini kuwa urafiki ni upendo wa dhati, kushirikiana kila kitu, na kuwa pamoja “milele”.

Tunakumbuka tulivyochora majina ya marafiki wetu kwenye daftari na kuandika: “Best Friend Forever – BFF.” Lakini kadri tulivyokua, maisha yalitufunza kuwa si kila aliye karibu yako ni wako kweli.

Kuna Hadija, msichana aliyekuwa na rafiki yake Halima kwa miaka sita. Walifanya kila kitu pamoja, shopping, ibada, likizo, hata biashara walifungua pamoja. Siku Hadija alipogundua kuwa yuko kwenye matatizo makubwa ya kifamilia na kifedha, alimtafuta Halima lakini simu haikupokelewa, ujumbe haukujibiwa. Mwezi mmoja baadaye, Halima aliweka picha Instagram akiwa safari na marafiki wapya, akiwa na tabasamu ambalo Hadija hajawahi kuona kwake.

Na huo ni mwanzo tu.

Uso Mbili wa Urafiki wa Kisasa:

Urafiki wa sasa umekuwa kama biashara isiyo rasmi, watu wanaingia kwa faida, si kwa upendo. Ni kama unapanda mti ukitarajia kivuli, lakini unapomaliza, mtu anauchuna matunda na kukukimbia.

Wengi wako kwako kwa sababu:

·       Unawasaidia kifedha

·       Unawapa ushauri

·       Unatoa muda wako

·       Una jina au ushawishi

·       Unawafariji wanapoumizwa

Lakini siku ukiwa umevunjika, wamechoka, au huna cha kutoa watatoweka bila majibu.

Unakumbuka ulivyomkopesha rafiki yako pesa kwa haraka, bila maandishi? Leo akikupita barabarani anageuza uso. Ule uliyeshiriki naye siri zako, leo anamwambia mwingine akisema, “hata mimi nilijua hajiwezi.”

Ishara za Marafiki Bandia (Red Flags):

1. Marafiki wa Matukio Tu

Wanakuja kwenye harusi, wanaku-tag kwenye birthday yako, lakini hawajui unaumwa. Hawajui ulihangaika kutafuta kodi ya nyumba, hawajui ulikosa mlo siku tatu. Kwao, maisha ni ya juu juu tu.

2. Wanaoshindana Badala ya Kushirikiana

Unapofanikiwa, wananyamaza. Wanashindwa hata kusema “hongera.” Badala yake, wanajaribu kukuiga au kukukosoa kisiri wakisema, “siyo lazima kujionyesha sana.”

3. Marafiki wa Siri

Ukisema kitu mbele yao leo, kesho unakisikia kwa watu wengine. Wanavaa tabasamu, lakini wana mdomo usiofungwa. Ukikaa nao muda mrefu, unajikuta umejaa hofu si kwa sababu ya woga, bali kwa sababu huna uhakika kama kesho utavikwa aibu.

4. Wanapenda Kupokea, Hawajui Kutoa

Unapoitwa rafiki, unaitwa mshirika. Lakini wengine wanaona urafiki kama mto wa kupokea msaada tu. Hawakumbuki hata kukuuliza kama upo salama.

Urafiki wa Kweli Upo – Lakini Ni Adimu:

Ndiyo. Urafiki wa kweli upo. Unaweza ukachelewa kuuona, lakini ukipatikana ni kama neema.

Rafiki wa kweli ni yule anayekukumbuka bila sababu. Anakutumia ujumbe usiku wa manane kuuliza, “Uko salama?”
Ni yule anayejua kuwa hucheki, lakini anakaa kimya tu kukusikiliza.
Ni yule anayelipa nauli ili akusindikize hospitali bila kukulalamikia.
Ni yule anayekuombea kimya kimya bila kukwambia, “nimekuombea.”

Namna ya Kutambua na Kulinda Urafiki wa Kweli:

1.      Angalia Wakati wa Shida: Wakati unapoumia au unaposhindwa – angalia nani anabaki.

2.      Tambua Nafsi ya Mtu: Marafiki wa kweli hawawezi kuwa watu wasio na huruma. Angalia utu, si ustadi wa maneno.

3.      Jifunze Mipaka: Usimruhusu kila mtu aingie kwenye maisha yako ndani sana. Tafuta waliothibitishwa kwa vitendo.

4.      Rafiki wa Kweli Anakuambia Ukweli: Haogopi kukusema ukienda kinyume. Anakujali zaidi kuliko anavyokupendeleza.

5.      Mshirikishe Mungu: Maombi huonyesha mengi usiyoyaona kwa macho. Mwombe Mungu akupe watu wa kweli.

Ushauri wa Maisha – Usiishi kwa Kivuli cha Urafiki Bandia:

Kuna watu wanabaki kwenye maisha yetu kama sumu ya taratibu. Wanapunguza thamani yetu, wanadhoofisha ndoto zetu, wanapandikiza hofu na mashaka. Huo si urafiki ni mzigo.

Achilia waliokuumiza, lakini usijisahau tena. Jifunze. Kua. Tazama upya. Usitafute wengi tafuta wa kweli mmoja, ni bora kuliko kundi la waigizaji.

Watu Wanabadilika Lakini Ukweli Haubadiliki. Urafiki wa kweli hautengenezwi kwa picha nzuri au maneno matamu. Hutengenezwa kwa wakati, maumivu, msamaha, na uaminifu. Wengine walikuja kukutumia, lakini wachache walikuja kukusaidia. Siku ukipata wa pili, mshikilie kwa moyo wote, kwa sababu katika dunia hii yenye kelele, kupata rafiki wa kweli ni sawa na kupata hazina.

Palubongo tunasema hivi: “Jipe nafasi ya kupendwa na watu wa kweli. Usihofie kupoteza marafiki feki, hofu ya kweli ni kuishi nao bila kujua.”

**Je, nawe una uzoefu wa aina hii? Tueleze kupitia maoni hapa chini au tuma ujumbe kupitia WhatsApp yetu. Simama nasi – sisi ni sauti yako._ 💬❤️_


Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Maisha: Safari Yenye Maswali Zaidi Kuliko Majibu

  Karibu sana kwenye blogu yangu! Leo naandika chapisho langu la kwanza – mwanzo wa safari ya mawazo, mazungumzo, na tafakari juu ya maisha. Maisha ni safari isiyo na ramani kamili, na cha kushangaza ni kwamba kila hatua tunayopiga huibua maswali mapya. Tunazaliwa bila kujua lolote, tunaingizwa kwenye mifumo ya maisha – shule, kazi, mahusiano, jamii – tukitarajiwa kuelewa kila kitu kwa haraka. Lakini ukweli ni kwamba, wengi wetu tunaishi tukijaribu kuelewa maana halisi ya maisha, tukitafuta majibu kwenye imani, mapenzi, kazi, au hata burudani. 🔍  Kwa Nini Naandika Blogu Hii? Ninaamini kuwa kila mtu ana hadithi, swali, au wazo ambalo linaweza kumgusa mtu mwingine. Blogu hii ni mahali pa kuzungumza kuhusu yale mambo ya kila siku – yaliyo wazi, yaliyo magumu, na hata yale ya kushangaza ambayo hayasemwi sana. Tutazungumzia imani, mitindo ya maisha, afya, historia, burudani, mapenzi, na yale mambo ambayo huenda hujawahi kuyawaza kabisa. Lengo si kutoa majibu yote, bali kuibua f...

WIVINA SYLIDION: SHUJAA WA MABADILIKO KWA MSICHANA WA KITANZANIA.

 Na Palubongo Team. Katika kona ya kaskazini-magharibi mwa Tanzania, mji wa Bukoba unafahamika kwa mandhari yake ya kuvutia, ziwa Victoria, na watu wenye upendo. Lakini kuna jina moja linang’aa zaidi ya mandhari, jina la msichana kijana, mwenye ndoto kubwa, moyo wa dhati, na kiu isiyozimika ya kuleta mabadiliko: Miss Wivina Sylidion . Alizaliwa na kulelewa Bukoba, mkoa wa Kagera, Wivina alionyesha mapema kuwa safari yake haitakuwa ya kawaida. Akiwa na Shahada ya Sayansi na Elimu, aliamua kutumia elimu yake kama chombo cha ukombozi hasa kwa wasichana walioko kwenye mazingira magumu. Aliona mapema jinsi jamii inavyowatizama wasichana kama dhaifu, na akaapa kuwa sehemu ya mabadiliko hayo. Wivina si tu mwalimu wa darasani bali ni mwalimu wa maisha. Kupitia taasisi aliyoianzisha kwa moyo wake mwenyewe “Binti na Kesho Yako” , amekuwa akiwafikia wasichana mashuleni, akiwapa elimu ya afya, maarifa ya kijamii, stadi za maisha, na matumaini. Anaamini kuwa msichana anapojitambua, jamii ...

Pua: Kiungo Kidogo Chenye Nguvu Kubwa Kuliko Tunavyodhani

K una msemo wa Kiswahili usemao, "Usidharau kidogo chenye maana." Lakini kwa bahati mbaya, wengi wetu tumekuwa tukidharau kiungo kimoja cha mwili wetu kwa sababu tu ni kidogo – pua . Tunaizungumzia mara chache, hatuitunzi ipasavyo, na mara nyingine tunaificha au kuifanyia upasuaji kwa sababu hatuipendi jinsi ilivyo. Lakini hebu tusimame kidogo na tujiulize: je, tunafahamu kweli nguvu iliyo ndani ya kiungo hiki kidogo? Tuangalie pamoja nguvu ya pua; 1. Mlango wa Maisha: Kupumua Kila pumzi tunayovuta huanza kwenye pua. Hapo ndipo maisha huingia. Bila hewa, hakuna uhai. Lakini si tu kuvuta na kutoa hewa – pua huchuja vumbi, vijidudu, na hata unyevu wa hewa kabla haijafika kwenye mapafu. Ikiwa tungekosa pua, mapafu yetu yangekuwa kwenye hatari kubwa sana kila tunapopumua. 2. Hisia Zinazoamsha Kumbukumbu Hebu fikiria harufu ya chakula cha nyumbani – labda wali wa nazi, au samaki wa kupaka unaopikwa na mama. Au harufu ya mvua ya kwanza kunyesha ardhini. Au hata manukato ...