Ruka hadi kwenye maudhui makuu

“Mwanga Wako Bado Unakuja: Hadithi Yako Haijaisha”


 

"Nilifikiria kuwa ifikapo miaka 30 nitakuwa na biashara yangu kubwa, familia yangu, nyumba yangu ya ndoto… lakini sasa nipo 35, sina chochote. Nimechoka. Najiona nimechelewa.”


Labda na wewe unajisemea hivi kila siku. Pengine kila jioni unatazama dari ukijilaumu, ukijilinganisha na wale mliomaliza shule pamoja ambao sasa wana magari yao, familia zao, au maisha mazuri ambayo wewe bado unayaota tu.

“Nilizaliwa kwenye familia yenye shida, nimesoma kwa shida, nimesota kwa miaka mingi, na sasa naona miaka inasonga… na bado sijaona hata mwanga wa ndoto zangu. Yani Nimechelewa sana kufanikiwa!”
Hapana ndugu yangu. Hujachelewa. Bado hujachelewa kabisa.

Tumekuwa tukijiambia na kujiapiza mambo mengi sana, Lakini maisha hayana “ratiba ya darasani.” Maisha yana mitihani, majaribu, magumu, na changamoto zisizotarajiwa. Na kwa bahati mbaya, yanatokea hasa pale ambapo tulitarajia mwanga.

Wengine wetu tumetoka kwenye familia masikini, hatukuwa na walimu wa kutufundisha maisha, hatukuwa na mfano wa kuigwa. Wengine tunaishi kwenye jamii yenye imani potofu ambapo mtu anaambiwa hawezi kufanikiwa kwa sababu ya ukoo wake, jina lake, historia ya familia, au unaambiwa “Ulikaliwa na mizimu”, “Familia yenu ni ya watu waliolaaniwa.”

Lakini leo, nataka nikuambie kwa sauti ya matumaini: HUJACHELEWA.

kuna vijana waliopitia haya haya, na leo wanang'ara. Hapa kuna mifano hai, ya kwetu Afrika na si hadithi za mbali:

1. William Kamkwamba – Malawi (alifanikiwa akiwa na miaka 14)

Aliwahi kuishi kwenye kijiji kisicho na umeme. Alijifunza kutoka kwenye vitabu vya zamani vya fizikia vilivyotupwa. Akajenga turbine ya upepo kwa kutumia mabaki ya vyuma na mashine chakavu. Leo, anazunguka dunia kama mhandisi na mhamasishaji wa sayansi.

2. Strive Masiyiwa – Zimbabwe

Alilelewa na mama peke yake baada ya baba kufariki. Alishindwa mara nyingi kuanzisha kampuni ya simu nchini kwake. Serikali ilimkataa mara kwa mara. Baada ya miaka 5 ya kesi mahakamani, alipata leseni ya kwanza ya simu. Leo ndiye mwanzilishi wa Econet Wireless, akiwa bilionea na mmoja wa wafadhili wakubwa Afrika.

3. Brian Mwenda – Kenya

Kijana ambaye hakuwa na shahada ya sheria lakini aliweza kuwakilisha watu mahakamani kwa mafanikio makubwa. Hali yake ilitokana na akili, bidii, na kupenda kujifunza. Wakati wenzake walipata msaada, yeye alipata dharau—lakini leo anaungwa mkono kimataifa kwa kipaji chake.

Wapo vijana wengi na watu mashuhuri ambao nisingeweza kuwaandika wote. Hivyo ndugu yangu nataka nikupe moyo kuwa bado HUJACHELEWA.

Mafanikio Hayana Umri Maalum.

Watu wengi waliotokea kuwa mashujaa wa dunia hii hawakufanikiwa kwa wakati ule unaodhani ndio "sahihi." Angalia mifano hii:

  • Colonel Sanders alianza KFC akiwa na miaka 65 baada ya kufutwa kazi mara kadhaa.
  • Oprah Winfrey alikumbwa na unyanyasaji wa kingono akiwa mtoto lakini leo ni mmoja wa wanawake mashuhuri duniani.
  • Morgan Freeman alianza kupata umaarufu akiwa na miaka 52.
  • Jack Ma alikataliwa kazi zaidi ya mara 30 lakini akaja kuanzisha Alibaba, kampuni kubwa ya e-commerce.

Unaona? Mafanikio hayafuati saa ya mkononi. Mafanikio huja kwa wakati wake. Na pengine saa yako ya dhahabu inakaribia kuonesha majira yako.

Kwa Nini Nasisitiza kuwa Bado Hujachelewa?

  • Kwa sababu bado una pumzi. Pumzi ni tiketi ya mabadiliko.
  • Kwa sababu unajitambua sasa. Kujitambua ni hatua kubwa ya kuelekea kwenye mafanikio.
  • Kwa sababu kila siku mpya ni nafasi mpya.

Waliowahi kufanikiwa si kwa sababu walikuwa bora kuliko wewe, bali kwa sababu:

1.      Walikubali hali yao lakini hawakubaki hapo.

2.      Waliamka kila siku wakijua hakuna atakayewasaidia isipokuwa wao wenyewe.

3.      Walijifunza, hata kama haikuwa darasani.

4.      Walikubali kupoteza usingizi, raha, marafiki… ili wafike walipotaka.

Ushauri Kwa Kijana wa Kiafrika Aliyekata Tamaa:

  1. Tafuta Maarifa Mpya;
    Elimu haina mwisho. Jifunze kitu kipya kila wiki iwe ni kupitia YouTube, vitabu, kozi fupi, au mentor wa karibu. Kila maarifa mapya ni chombo cha ushindi.
  2. Kataa Imani Potofu;
    Sio kweli kwamba huwezi kufanikiwa kwa sababu ukoo wako ni maskini. Historia haikufungi, bali inakupa msingi wa kujenga historia mpya.
  3. Toa Jasho, Sio Malalamiko;
    Maisha hayambatani na huruma. Kama huna ajira, jiajiri. Kama huna mtaji, tafuta ujuzi. Kama huna msaada, tafuta marafiki wenye maono.
  4. Lenga Fursa, Usilenge Majuto;
    Badala ya kuangalia nyuma ulipokosea, angalia mbele unapoweza kwenda. Fursa zipo mitandaoni, kwenye maonyesho, kwenye mazungumzo ya watu, jitokeze, jiwasilishe.
  5. Zunguka na Watu Sahihi;
    Marafiki zako ni kama mbolea au sumu. Tafuta wale wanaokutia nguvu, wanaokuambia “inawezekana”, si wale wanaokushusha na kukuambia “tulizana tu maisha ndio haya.”
  6. Omba Lakini Pia Tenda;
    Mungu hasaidii wale wanaolala tu. Anasaidia wale wanaojitahidi. Maombi yawe na matendo.

7.      Amua leo; Usiseme “nitajaribu mwakani.” Mwaka huo huwezi kuuona kama huanzi leo.

Ndiyo, maisha yanaweza kuwa magumu. Ndiyo, unaweza kuwa umechelewa kwa ratiba zako mwenyewe. Lakini hujachelewa kwa mpango wa Mungu. Hujachelewa kwa wakati wako wa pekee.

Inawezekana hujasoma chuo kikuu. Inawezekana hukupata A kwenye matokeo. Labda baba yako ni mlevi, au mama yako alikuacha ukiwa mdogo. Labda umejaribu kuanzisha biashara mara 4, zote zikafa. Labda marafiki zako wote wamepata kazi, wameoa, wameolewa… na wewe bado unapanga mpango wa kesho. Kila mtu ana saa yake. Wakati wako utafika. Endelea kupambana. Endelea kujifunza. Endelea kuamini. Hujachelewa.

Mtu aliyepanda mti mwaka jana, leo anakula matunda. Wewe ukipanda leo, utakula miaka ijayo. Usikae ukitazama miti ya watu wengine. Panda yako. Mwagilia yako. Itaota.
Na siku ikifika, utaangalia nyuma na kusema:

"Nilivumilia. Nilipambana. Na sasa, nimefika. HUJACHELEWA."

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Maisha: Safari Yenye Maswali Zaidi Kuliko Majibu

  Karibu sana kwenye blogu yangu! Leo naandika chapisho langu la kwanza – mwanzo wa safari ya mawazo, mazungumzo, na tafakari juu ya maisha. Maisha ni safari isiyo na ramani kamili, na cha kushangaza ni kwamba kila hatua tunayopiga huibua maswali mapya. Tunazaliwa bila kujua lolote, tunaingizwa kwenye mifumo ya maisha – shule, kazi, mahusiano, jamii – tukitarajiwa kuelewa kila kitu kwa haraka. Lakini ukweli ni kwamba, wengi wetu tunaishi tukijaribu kuelewa maana halisi ya maisha, tukitafuta majibu kwenye imani, mapenzi, kazi, au hata burudani. 🔍  Kwa Nini Naandika Blogu Hii? Ninaamini kuwa kila mtu ana hadithi, swali, au wazo ambalo linaweza kumgusa mtu mwingine. Blogu hii ni mahali pa kuzungumza kuhusu yale mambo ya kila siku – yaliyo wazi, yaliyo magumu, na hata yale ya kushangaza ambayo hayasemwi sana. Tutazungumzia imani, mitindo ya maisha, afya, historia, burudani, mapenzi, na yale mambo ambayo huenda hujawahi kuyawaza kabisa. Lengo si kutoa majibu yote, bali kuibua f...

WIVINA SYLIDION: SHUJAA WA MABADILIKO KWA MSICHANA WA KITANZANIA.

 Na Palubongo Team. Katika kona ya kaskazini-magharibi mwa Tanzania, mji wa Bukoba unafahamika kwa mandhari yake ya kuvutia, ziwa Victoria, na watu wenye upendo. Lakini kuna jina moja linang’aa zaidi ya mandhari, jina la msichana kijana, mwenye ndoto kubwa, moyo wa dhati, na kiu isiyozimika ya kuleta mabadiliko: Miss Wivina Sylidion . Alizaliwa na kulelewa Bukoba, mkoa wa Kagera, Wivina alionyesha mapema kuwa safari yake haitakuwa ya kawaida. Akiwa na Shahada ya Sayansi na Elimu, aliamua kutumia elimu yake kama chombo cha ukombozi hasa kwa wasichana walioko kwenye mazingira magumu. Aliona mapema jinsi jamii inavyowatizama wasichana kama dhaifu, na akaapa kuwa sehemu ya mabadiliko hayo. Wivina si tu mwalimu wa darasani bali ni mwalimu wa maisha. Kupitia taasisi aliyoianzisha kwa moyo wake mwenyewe “Binti na Kesho Yako” , amekuwa akiwafikia wasichana mashuleni, akiwapa elimu ya afya, maarifa ya kijamii, stadi za maisha, na matumaini. Anaamini kuwa msichana anapojitambua, jamii ...

Pua: Kiungo Kidogo Chenye Nguvu Kubwa Kuliko Tunavyodhani

K una msemo wa Kiswahili usemao, "Usidharau kidogo chenye maana." Lakini kwa bahati mbaya, wengi wetu tumekuwa tukidharau kiungo kimoja cha mwili wetu kwa sababu tu ni kidogo – pua . Tunaizungumzia mara chache, hatuitunzi ipasavyo, na mara nyingine tunaificha au kuifanyia upasuaji kwa sababu hatuipendi jinsi ilivyo. Lakini hebu tusimame kidogo na tujiulize: je, tunafahamu kweli nguvu iliyo ndani ya kiungo hiki kidogo? Tuangalie pamoja nguvu ya pua; 1. Mlango wa Maisha: Kupumua Kila pumzi tunayovuta huanza kwenye pua. Hapo ndipo maisha huingia. Bila hewa, hakuna uhai. Lakini si tu kuvuta na kutoa hewa – pua huchuja vumbi, vijidudu, na hata unyevu wa hewa kabla haijafika kwenye mapafu. Ikiwa tungekosa pua, mapafu yetu yangekuwa kwenye hatari kubwa sana kila tunapopumua. 2. Hisia Zinazoamsha Kumbukumbu Hebu fikiria harufu ya chakula cha nyumbani – labda wali wa nazi, au samaki wa kupaka unaopikwa na mama. Au harufu ya mvua ya kwanza kunyesha ardhini. Au hata manukato ...