Hakika, mazungumzo yetu na MC Franklin yalikuwa zaidi ya mahojiano – yalikuwa safari ya moyo, changamoto, imani, na
mafanikio. Tunapokuletea simulizi hii kupitia Palubongo, jiandae kuguswa
na maisha halisi ya kijana huyu mahiri, ambaye kwa sasa anatambulika kama mmoja
wa washehereshaji chipukizi, wachapakazi, wenye mvuto na ari isiyozuilika.
Katika jiji lenye pilikapilika nyingi la Dar
es Salaam, tulikutana na kijana mmoja mwenye mwanga wa kipekee. Franklin
Rwejuna maarufu kama MC FRANKLIN – mhaya kwa kabila, mzaliwa wa Hospitali ya Mwananyamala –
alitufungulia moyo wake, akitueleza safari yake ya maisha kwa namna ya kuvutia,
yenye hisia, na iliyojaa mafunzo kwa kila kijana anayesaka mafanikio ya kweli.
Utoto na Malezi ya Maadili
Franklin alikulia Sinza, Dar es Salaam, akiwa
mtoto wa kwanza kati ya wawili, akifuatwa na dada yake. Wazazi wake walimlea
kwa mikono yote miwili – mama akiwa ni taswira ya huruma, upole na imani, huku
baba akiwa ni mfano halisi wa nidhamu, ukakamavu na uchapakazi. "Mama
alikuwa akinisisitiza sana kusali na kumtanguliza Mungu. Baba yangu hakuwa mtu
wa mzaha – alikuwa mkali kwenye mambo mabaya lakini mwenye maono ya
kunijenga," alituambia kwa sauti ya kumbukumbu iliyojaa hisia.
Alijifunza mapema kuwa maisha yanahitaji
mchanganyiko wa bidii na kumtumainia Mungu msingi ambao hadi leo amekuwa nao
kama dira ya mafanikio.
Kupitia Giza la Machungu na Mwanga wa
Tumaini
Wakati Franklin akiwa kidato cha pili, dunia
ilimgeuka ghafla. Baba yake, nguzo ya familia, alifariki. Kwa kijana aliyekuwa
bado mdogo, kilikuwa kipindi kigumu kisichoelezeka kwa maneno. "Nilijikuta
na jukumu la kuwa mwanaume wa familia. Maisha yalibadilika sana – hata mahitaji
ya msingi yalikuwa vigumu kupatikana," alisimulia kwa sauti iliyojaa utu
uzima uliochipuka mapema.
Aliwahi kufikiria kuokota chupa za plastiki
ili kupata pesa, lakini mama alimzuia. Badala yake, akaanza kuuza uji katika
soko la Rangi Tatu, akihangaika kuhakikisha familia haijakosa kabisa. Lakini
pamoja na yote, hakuwahi kuacha ndoto zake. Hatimaye alifaulu kujiunga na Chuo
Kikuu cha Dodoma, akibeba ushahidi wa kwamba bidii na imani ni nguzo
zinazoshinda yote.
Kazi Yake ya Uanashehereshaji na
Ualimu
Leo hii, Franklin ni mwalimu na pia MC maarufu
kwenye sherehe mbalimbali, hasa za harusi. "Kazi ya kuwa MC imenipa nafasi
ya kuona maisha ya watu kwa jicho la karibu – ndoa, familia, upendo, migogoro,
na furaha. Kila harusi ninayoiongoza huwa somo jipya."
Anaingiza ubunifu, hisia, na weledi katika
kazi yake – akiiweka hadhira katika hali ya furaha na mshikamano. “Sio kazi ya
kusimama na kuongea tu, ni sanaa ya kugusa moyo wa mtu.”
Upendo, Familia na Maisha ya Kijamii
Kuhusu masuala ya mapenzi, Franklin ana
mtazamo wa kipekee. Anaamini kuwa uaminifu, uvumilivu, na ubunifu ni misingi
mikuu ya uhusiano mzuri. Ana mpenzi ambaye anamsifia kwa mapenzi ya dhati,
uelewa, na mshikamano – jambo ambalo linampa nguvu hata zaidi katika maisha.
Anasema, “Mapenzi ni kama muziki – yanahitaji
mziki mzuri, mdundo sahihi, na uvumilivu kusikiliza hadi mwisho. Na zaidi ya
yote, ni lazima mpenzi wako awe rafiki.”
Ujumbe kwa Vijana
Franklin aliwaachia vijana wa Tanzania ujumbe
mzito lakini uliojaa matumaini. "Mafanikio siyo magari au nyumba kubwa tu.
Mafanikio ni kutoka hatua ya chini kwenda juu – hata kama ni hatua moja tu.
Ujipime mwenyewe, usijiweke kwenye mizani ya watu."
Alisisitiza kuwa hakuna maisha mepesi, lakini
Mungu akitangulia, na wewe ukijituma, kila mlango unaweza kufunguka.
"Usikate tamaa. Hata ukiwa kwenye giza nene, endelea kutembea – kuna nuru
mbele."
Franklin Rwejuna ni mfano wa jinsi gani
juhudi, imani, na maadili vinaweza kumtoa mtu kutoka kwenye hali ngumu kabisa
na kumfikisha mahali pa heshima. Kupitia Palubongo, tunatambua juhudi na
safari ya kila kijana mwenye ndoto – kama Franklin – ambaye anafanya maisha
kuwa bora kwa kugusa mioyo ya watu kila siku.
Tunaamini, huu ni mwanzo tu kwa Franklin.
Dunia bado haijamwona kikamilifu. 🌟

Maoni
Chapisha Maoni