Ruka hadi kwenye maudhui makuu

Kwa Nini Tunaogopa Kuwa Peke Yetu?


 

"Upweke siyo laana, ni nafasi ya kuongea na nafsi yako kwa sauti ya ndani ambayo ulimwengu hauwezi kusikia."

Zamani za kale, kabla ya kuwepo kwa magereza, jamii zilitumia adhabu za moja kwa moja kama kufukuzwa kwenye kijiji, kuchapwa viboko au hata kuuawa kwa makosa fulani. Lakini takribani miaka 3,000 iliyopita huko Mesopotamia (leo ni Iraq), ilibuniwa wazo la kwanza la kumtenga mtu kwa muda kama adhabugereza. Lengo halikuwa tu kumwadhibu, bali kumtenga, ili atafakari makosa yake na ajirekebishe.

Katika karne ya 18, mfumo wa magereza ulianza kubadilika huko Ulaya na Amerika. Walianza kutumia "solitary confinement" yaani kumweka mfungwa peke yake kabisa bila kuzungumza na mtu yeyote kwa muda mrefu. Lengo lilikuwa kumlazimisha akutane na nafsi yake, akae kimya na kufikiri. Wanafikra wa wakati huo waliamini kuwa ukimya na upweke vina nguvu ya kumrekebisha mtu, lakini pia waligundua kuwa ndiyo adhabu kali zaidi kisaikolojia.

Leo hii, hata bila kufungwa gerezani, wengi wetu tunaishi kwa kuogopa sana kuwa peke yetu. Lakini kwanini? Ni nini hasa kinatufanya tuone kuwa upweke ni kama kifungo cha roho?

~~~~~~~~~~~

Kulikuwa na kijana mmoja aitwaye Baraka, aliyekulia kijijini kwetu kule Tanga. Alikuwa na sauti nzuri, akili nyingi, na haikuwa nadra kumsikia akiendesha michezo ya kuigiza kwenye mikutano ya vijana. Lakini kulikuwa na jambo moja alilolikwepa kila mara kama ambavyo vijana wengi wanalikwepa, kuwa peke yake.

Alijaza siku zake kwa watu, kelele, miziki, mahusiano ya haraka, vikao na safari. Hakuwa anaweza kukaa kimya, wala kufurahia saa moja bila mtu pembeni.

Lakini bahati au mkosi ukamjia, ghafla alipoteza kazi, mpenzi wake akaondoka, simu zikawa kimya. Marafiki ndugu na hata vijana wenzie walipunguza kujumuika nae. Ndipo alikutana na mtu aliyekuwa anamkimbia maisha yote, nafsi yake.

Nafsi yake ndiyo ukweli wake halisi, hauku - mdanganya, wala haukumpa furaha isiyo ya kweli. Baraka alikuwa na sonona sana kwa muda mrefu kwasababu tu alikuwa mpweke.

Katika jamii za Kiafrika, mshikamano na ushirika ni maadili muhimu sana. Mtu anayeishi peke yake huonekana kuwa na matatizo. Mwanamke asiyeolewa huonewa huruma. Kijana asiye na marafiki anaambiwa "anatabia mbaya sana," kana kwamba upweke ni laana.

Lakini ukweli ni kwamba: Tunaogopa kuwa peke yetu kwa sababu upweke hutuonyesha kile tulichojificha nacho.

Upweke unavua kila kisingizio. Hakuna sifa, hakuna vicheko vya bandia, hakuna likes za mitandaoni, ni wewe na hali yako ya ndani. Hii ndiyo maana hata jela, sehemu ya kutisha zaidi ni ya pekee yaani kifungo cha upweke.

Siri ya Upweke: Wema wake na Ubaya wake

Upweke ni kioo kisichosema uongo. Kinaonyesha sura yako halisi siyo ile ya kamera au ya mitandao. Kinaonyesha hofu zako, matarajio yako, ndoto ulizoacha, makosa yako ya zamani, na ukimya wako wa ndani.

Kwa hiyo, si kwamba watu wanaogopa kuwa pekee, wanaogopa kukutana na nafsi zao.

Lakini Vipi Kama Upweke ni Zawadi Iliyofichwa?

Historia inaonyesha kuwa watu wengi waliotenda mambo makubwa walipitia kipindi cha upweke.

  • Nelson Mandela alikaa miaka 27 gerezani, sehemu kubwa akiwa peke yake. Akiwa huko alisoma, alitafakari, akaandika barua na kujifunza lugha za Afrikaans ambayo ilikuwa hatua muhimu ya kuja kupatanisha Afrika Kusini.
  • Wangari Maathai, mama shupavu kutoka Kenya, alikataliwa, kudhalilishwa na kutengwa. Lakini aliendelea kupanda miti peke yake hadi dunia ikamtambua.
  • Yesu Kristo, alitumia muda mwingi porini akiwa peke yake kabla ya kuanza huduma yake.



Hata nyumbani, Mama Nuru wa kijiji chetu, baada ya kufiwa na mume wake miaka 30 iliyopita, alihisi dunia imemwacha. Lakini upweke wake ukawa nguvu. Alianza kufuga, kulima mitishamba, sasa watu wanamsaka kwa uponyaji wa asili. Yote yalitokana na muda aliotumia akiwa mwenyewe na Mungu.

Madhara ya Kuogopa Kuwa Peke Yako;

  • Kukosa kujijua na kujitambua
  • Kuweka tegemeo kubwa kwa wengine kisaikolojia
  • Kuingia kwenye mahusiano yasiyo sahihi ili kuepuka upweke
  • Kuzama kwenye kelele za mitandao ya kijamii hadi kupotea kiroho na kiakili

Jinsi ya Kugeuza Upweke Kuwa Nguvu;

  1. Tenga muda wa kimya kila siku – japo dakika 10, usikilize moyo wako.
  2. Andika hisia zako – kujieleza kunaondoa machungu ya ndani.
  3. Soma na tafakari – vitabu ni marafiki wasiohukumu.
  4. Tembea bila simu – tafuta mandhari ya asili; mitende, bahari, au mlima, hapo ndipo nafsi huongea.
  5. Jenga uhusiano wa kiroho – sala, dua, au kutafakari ni njia ya kuponya nafsi.

Upweke Siyo Kifungo, Ni Daraja

Upweke unaweza kuwa gereza, lakini kwa mwenye maarifa, ni daraja la kuelekea kwenye nuru. Ni wakati wa kukua, kujijua, na kutulia. Kama jamii, tunapaswa kuwasaidia vijana wetu wasione upweke kama udhaifu bali kama fursa.

Je, wewe umewahi kuogopa kuwa pekee? Au upo katika kipindi cha ukimya kwa sasa? Ni nini ulichojifunza ukiwa peke yako?
Tuandikie kwenye maoni au tuma ujumbe kupitia WhatsApp ya Palubongo.

"Palubongo – Tunasikiliza, Tunahisi, Tunaguswa." 🖤

 

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Maisha: Safari Yenye Maswali Zaidi Kuliko Majibu

  Karibu sana kwenye blogu yangu! Leo naandika chapisho langu la kwanza – mwanzo wa safari ya mawazo, mazungumzo, na tafakari juu ya maisha. Maisha ni safari isiyo na ramani kamili, na cha kushangaza ni kwamba kila hatua tunayopiga huibua maswali mapya. Tunazaliwa bila kujua lolote, tunaingizwa kwenye mifumo ya maisha – shule, kazi, mahusiano, jamii – tukitarajiwa kuelewa kila kitu kwa haraka. Lakini ukweli ni kwamba, wengi wetu tunaishi tukijaribu kuelewa maana halisi ya maisha, tukitafuta majibu kwenye imani, mapenzi, kazi, au hata burudani. 🔍  Kwa Nini Naandika Blogu Hii? Ninaamini kuwa kila mtu ana hadithi, swali, au wazo ambalo linaweza kumgusa mtu mwingine. Blogu hii ni mahali pa kuzungumza kuhusu yale mambo ya kila siku – yaliyo wazi, yaliyo magumu, na hata yale ya kushangaza ambayo hayasemwi sana. Tutazungumzia imani, mitindo ya maisha, afya, historia, burudani, mapenzi, na yale mambo ambayo huenda hujawahi kuyawaza kabisa. Lengo si kutoa majibu yote, bali kuibua f...

WIVINA SYLIDION: SHUJAA WA MABADILIKO KWA MSICHANA WA KITANZANIA.

 Na Palubongo Team. Katika kona ya kaskazini-magharibi mwa Tanzania, mji wa Bukoba unafahamika kwa mandhari yake ya kuvutia, ziwa Victoria, na watu wenye upendo. Lakini kuna jina moja linang’aa zaidi ya mandhari, jina la msichana kijana, mwenye ndoto kubwa, moyo wa dhati, na kiu isiyozimika ya kuleta mabadiliko: Miss Wivina Sylidion . Alizaliwa na kulelewa Bukoba, mkoa wa Kagera, Wivina alionyesha mapema kuwa safari yake haitakuwa ya kawaida. Akiwa na Shahada ya Sayansi na Elimu, aliamua kutumia elimu yake kama chombo cha ukombozi hasa kwa wasichana walioko kwenye mazingira magumu. Aliona mapema jinsi jamii inavyowatizama wasichana kama dhaifu, na akaapa kuwa sehemu ya mabadiliko hayo. Wivina si tu mwalimu wa darasani bali ni mwalimu wa maisha. Kupitia taasisi aliyoianzisha kwa moyo wake mwenyewe “Binti na Kesho Yako” , amekuwa akiwafikia wasichana mashuleni, akiwapa elimu ya afya, maarifa ya kijamii, stadi za maisha, na matumaini. Anaamini kuwa msichana anapojitambua, jamii ...

Pua: Kiungo Kidogo Chenye Nguvu Kubwa Kuliko Tunavyodhani

K una msemo wa Kiswahili usemao, "Usidharau kidogo chenye maana." Lakini kwa bahati mbaya, wengi wetu tumekuwa tukidharau kiungo kimoja cha mwili wetu kwa sababu tu ni kidogo – pua . Tunaizungumzia mara chache, hatuitunzi ipasavyo, na mara nyingine tunaificha au kuifanyia upasuaji kwa sababu hatuipendi jinsi ilivyo. Lakini hebu tusimame kidogo na tujiulize: je, tunafahamu kweli nguvu iliyo ndani ya kiungo hiki kidogo? Tuangalie pamoja nguvu ya pua; 1. Mlango wa Maisha: Kupumua Kila pumzi tunayovuta huanza kwenye pua. Hapo ndipo maisha huingia. Bila hewa, hakuna uhai. Lakini si tu kuvuta na kutoa hewa – pua huchuja vumbi, vijidudu, na hata unyevu wa hewa kabla haijafika kwenye mapafu. Ikiwa tungekosa pua, mapafu yetu yangekuwa kwenye hatari kubwa sana kila tunapopumua. 2. Hisia Zinazoamsha Kumbukumbu Hebu fikiria harufu ya chakula cha nyumbani – labda wali wa nazi, au samaki wa kupaka unaopikwa na mama. Au harufu ya mvua ya kwanza kunyesha ardhini. Au hata manukato ...